Thursday 12 July 2012

NAIBU WAZIRI


Joseph Lyimo,Mirerani
NAIBU Waziri wa Nishati na Madini,Stephen Masele ameiamuru kampuni ya TanzaniteOne kuacha kumwaga maji kwenye migodi ya wachimbaji wadogo wa madini ya Tanzanite wa mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.

Akizungumza na uongozi wa kampuni hiyo,Masele ambaye ni Naibu Waziri anayeshughulikia madini aligeuka na kuwa mkali mithili ya mbogo wakati akizungumzia suala hilo kwa viongozi wa kampuni hiyo.

Naibu waziri alitoa amri hiyo baada ya kuelezwa na wachimbaji wadogo alipofanya ziara ya kutembelea migodi yao kuwa kampuni hiyo inawamwagia maji mgodini na alipotoa amri hiyo gari lake lilisukumwa na wachimbaji hao.

“Sawa hawa ni wawekezaji lakini Serikali haipo tayari kuona wachimbaji wadogo wananyanyaswa katika nchi yao hivyo nimeiamuru kampuni hiyo kusitisha mara moja kumwaga maji hayo,” alisema Masele.

Hata hivyo,Mwenyekiti wa kampuni ya TanzaniteOne,Ammi Mpungwe alimthibitishia Masele kuwa kampuni yake haimwagi maji kwenye migodi ya wachimbaji wadogo ila maji hayo yanatoka yenyewe kwenye mgodi wa TanzaniteOne. 

Mpungwe alisema maji hayo hutoka nyenyewe kutokana na jiolojia ya miamba ilivyo kwenye mgodi wao wa Bravo ambao haufanyiwi kazi lakini kampuni hiyo haijawahi kumwaga maji kwenye migodi ya wachimbaji wadogo.

“Mheshimiwa waziri mimi nilikuwa balozi na nikastaafu kwa heshima zote,sasa siwezi kwenda jela leo kwa kosa la kukiuka sheria za nchi,mimi ni mzalendo sitakubali kuruhusu kampuni yetu imwage maji migodini,” alisema Mpungwe.

Pia,Naibu Waziri huyo aliitaka kampuni hiyo kusaidia huduma za jamii kama madawati shuleni,afya na maji kwenye kata zote nne za tarafa ya Moipo wilayani humo kuliko kuisaidia kata moja ya Naisinyai.

“Watanzania hawatatuelewa ikiwa kampuni hii inachimba madini ya Tanzanite yenye utajiri mkubwa wakati kata za jirani wanafunzi wanakaa  sakafuni,huduma za afya duni na barabara ya Kia-Mirerani ni ya vumbi,” alisema Masele.

Akizungumzia kuhusu hilo,Mpungwe alisema watajipanga kulitekeleza ila alisikitishwa na kitendo cha viongozi wa kilichokuwa kijiji cha Mirerani kukataa msaada wa zaidi ya sh12 milioni walizotoa kama msaada wa maendeleo mwaka 2000.

MWISHO.

No comments:

Post a Comment