Monday 29 January 2018

HALMASHAURI YA WILAYA YA MBULU YAPITISHA MPANGO WA BAJETI WA SHILINGI BILIONI 43.983

 Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, limepitisha shilingi bilioni 43.983 za mapendekezo ya mpango wa bajeti kwa mwaka wa fedha wa 2018/2019.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Hudson Kamoga, akizungumza baada ya kupitishwa bajeti hiyo, alisema vipaumbele vyake ni elimu, afya, maji, kilimo na mifugo.

Kamoga alisema bajeti hiyo imezingatia vipaumbele vya vijiji, kata, halmashauri, mkoa, mpango wa pili wa maendeleo ya Taifa na dira ya maendeleo ya Taifa ya mwaka 2025. 
 Alisema vipaumbele vingine ni mikakati na sera mbalimbali za kisekta, maelekezo mbalimbali ya viongozi wakuu wa kitaifa, na ahadi ya Rais John Magufuli alizozitoa wakati wa kampeni wilayani Mbulu.

Alisema halmashauri hiyo imejikita katika kuongeza mapato ya ndani kwa kuimarisha vyanzo vilivyopo, kubuni vyanzo vipya na kuimarisha mfumo wa kielectroniki. 
"Halmashauri imejikita katika mpango bora wa matumizi ya ardhi kwa makazi, biashara, viwanda vidogo, maeneo ya malisho ya mifugo, kilimo, hifadhi ya mazingira na uhifadhi wa vyanzo vya maji," alisema Kamoga.

Mbunge wa jimbo la Mbulu Vijijini, Flatei Massay alipongeza kupitishwa kwa bajeti hiyo ambayo imekidhi kuondoa changamoto mbalimbali.

Massay alisema bajeti hiyo imegusa sekta mbalimbali ikiwemo elimu ya msingi, sekondari, kilimo, mifugo, ushirika, umwagiliaji, afya na maji.

Alisema anatarajia wananchi wa jimbo hilo watapiga hatua kubwa ya maendeleo kupitia utekelezaji wa miradi ya mpango wa bajeti iliyopishwa na madiwani wa halmashauri ya wilaya hiyo.

Mwanasheria wa halmashauri hiyo, Honoratus Mulokozi alisema bajeti hiyo kabla ya kupitishwa imezingatia sheria namba 9 ya serikali za mitaa ya mwaka 1982.

Mulokozi alisema sheria hiyo ilifanyiwa marekebisho Januari mosi mwaka 2000 inayotaka kufuata sheria, kanuni na taratibu, wakati wa kuandaa bajeti.


No comments:

Post a Comment