Saturday 28 May 2016

OLE MILLYA KUANZISHA KAMATI YA MAENDELEO SIMANJIRO



Mbunge wa Jimbo la Simanjiro Mkoani Manyara, James Ole Millya amesema ataanzisha kamati ya wadau wa maendeleo ya Simanjiro, itakayoongozwa na aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Singida Parseko Kone. 

Ole Millya alisema hawezi kuwaweka kando wasomi wa wilaya hiyo, hivyo atawakumbatia kwani Simanjiro haiwezi kuendelea bila ushirikiano wa wadau mbalimbali wenye maono ya kuifikisha mbali.

Alisema ameshapata msaidizi wake, Joshua Kuney ambaye ni katibu wa mbunge hivyo kilichobakia ni kuhakikisha timu hiyo inakutana mara moja kwa kushirikiana na wazee wa mila watafanikisha maendeleo.



Diwani wa kata ya Naberera Haiyo Mamasita, alisema hivi sasa uchaguzi umeshapita hivyo kinachotakiwa ni kuhakikisha maendeleo ya wananchi yanapatikana ikiwemo huduma muhimu za kijamii za maji, elimu na afya.

“Changamoto kubwa iliyopo hivi sasa ni kuhakikisha suala zima la elimu linafanikiwa kwenye kata yetu ya Naberera na nitahakikisha wanafunzi waliokuwa wanakosa hiyo fursa wanafanikiwa,” alisema Mamasita.



Ole Millya alisema miongoni mwa wadau wa maendeleo na wasomi watakaokuwa kwenye kamati hiyo ambayo haitajadi itikadi za kisiasa ni mkuu wa wilaya ya Kakonko mkoani Kigoma Peter Toima na Katibu wa Chadema Simanjiro Frank Oleleshwa.

“Siwezi kuwakataa wasomi wa Simanjiro kwani tutashirikiana nao tupate maendeleo, nataka mwisho wa siku ikifika uchaguzi kama kunipa mnipe ninyi wenyewe na kama kuninyima mninyime wenyewe,” alisema Ole Millya. 

Alisema huwezi kufanikiwa maendeleo ya wananchi wa Simanjiro ili hali unaogopa kushirikiana na wasomi, kwani japokuwa wengine wapo nje ya eneo hilo lakini kupitia ushirikiano waliouanzisha watafanikisha mambo mengi.

No comments:

Post a Comment