Thursday, 15 June 2017

WATANZANIA WATAKIWA KUMUUNGA MKONO RAIS MAGUFULI KWENYE VITA YA KULINDA RASILIMALI



Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Hudson Kamoga amesema watanzania wanapaswa kumuunga mkono Rais John Magufuli kwenye vita ya kulinda rasilimali za nchi aliyoianzisha.

Kamoga aliyasema hayo juzi kwenye maadhimisho ya siku ya albino
duniani, ambayo  kimkoa ilifanyika kituo cha 4 Angle mji mdogo wa
Haydom na alimwakilisha mkuu wa mkoa huo Dk Joel Bendera.

Alisema vita ya kulinda rasilimali ya nchi inapaswa kuungwa mkono
kwani utajiri wa nchi ya Tanzania haulingani na hali halisi iliyopo
kutokana na watu wachache kupora utajiri kupitia madini mbalimbali.






Alisema ana imani Rais Magufuli na watanzania kwa ujumla watashinda vita ya kulinda rasilimali kwani kupitia ripoti ya pili ya makania imeonyesha namna wananchi wanyonge wanavyoibiwa.

“Pamoja na kuathimisha siku ya albino duniani tunapaswa kumuunga mkono Rais Magufuli katika vita hii ya kusimamia na kulinda rasilimali za nchi kupitia madini yetu kwani nia ya dhati ameionyesha,” alisema Kamoga.



 

Mwenyekiti wa chama cha maalbino mkoani Manyara, Joseph Masasi alisema wanakabiliwa na changamoto ya kutobaini idadi kamili ya watu wenye ualbino mkoani humo hivyo kukosa takwimu sahihi.

Masasi alisema tatizo hilo linasababisha hata kukitokea tatizo lolote
linalohitaji msaada kwao inakuwa vigumu kwani wengine wanakosa
kutokana na kutobainishwa kwa idadi yao katika wilaya za mkoa huo.

Alisema pia wanakabiliwa na tatizo la ukosefu wa mafuta maalum ya
kujipaka kwa watu wenye ualbino yanayowasaidia kila siku ili
wasiathiriwe na mionzi ya jua na kusababisha baadhi yao kuathirika.

“Pamoja na hayo tunashukuru kwenye mkoa wa Manyara hakuna matukio ya watu wenye ualbino kuuawa au kukatwa viungo na watu makatili ila kuna badhi ya matishio madogo madogo,” alisema Masasi.

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo Joseph Mandoo alisema halmashauri yao itaendelea kushirikiana na uongozi wa ualbino kwa ajili ya kuhakikisha wanatoa msaada unaohitajika kwa watu hao.

Mandoo alitoa wito kwa wazazi na walezi wenye watoto wenye ualbino kutowafisha ndani na badala yake wawafikishe kwenye sehemu husika ili pindi misaada itakapotolewa waweze kupatiwa.




MIZINGA YA NYUKI

Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe akikabidhi moja kati ya mizinga 50 kwa vikundi vya jamii ya wahadzabe wa Wilaya ya Mkalama Mkoani Singida.

Tuesday, 6 June 2017

WAFUGAJI WALIA NA UCHACHE WA VYUMBA VYA MADARASA NA WALIMU



Wanafunzi wa shule ya msingi Lesirwai, Kijiji cha Marwa Kata ya Ruvu
Wilayani Same Mkoani Kilimanjaro, wanakabiliwa na changamoto ya kusoma madarasa mawili wakitumia chumba kimoja.

Kutokana na uhaba wa madarasa, wanafunzi wa madarasa ya kwanza na la pili, la tatu na la nne, la tano na la sita, husoma kwenye chumba
kimoja huku wale wa darasa la saba wakitumia ofisi ya walimu.

Wakizungumza shuleni hapo, baadhi ya wananchi wa kijiji hicho
walidai kuwa shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 2014 ina wanafunzi wa
darasa la kwanza hadi la saba ila ina vyumba vinne tuu vya madarasa.

Mmoja kati ya wananchi hao,  Zacharia Leyani alisema japo kuwa jamii ya eneo hilo hivi sasa ina mwamko mkubwa lakini wanakwamishwa na miundombinu mibovu ya shule hiyo.

Alisema wanafunzi wanakuwa na wakati mgumu wa kufuatilia masomo kwa usahihi kwani wanakuwa wanafuatilia mafundisho mengine pindi wenzao wakiwa wanafundishwa na mwalimu.

“Chumba kimoja cha darasa hivi sasa wanafundishwa wanafunzi wa
madarasa mawili sasa sijui mwalimu atakuwa na mwamko gani wa
kufundisha tunaomba serikali iangalie hii hali,” alisema Leyani.

Mwalimu mkuu wa shule hiyo Tendwa Barnaba alithibisha wanafunzi hao kusoma kwenye chumba cha darasa moja kutokana na uhaba wa madarasa uliopo huku wanafunzi wa darasa la saba wakitumia ofisi .

Barnaba alisema pamoja na uchache wa vyumba vya madarasa, pia shule hiyo inakabiliwa na upungufu mkubwa wa walimu kwani japokuwa kuna wanafunzi 140 wapo walimu watatu pekee.

“Changamoto hizo zingepatiwa ufumbuzi tungepata moyo, tunaomba
tuongezewe vyumba vya madarasa na walimu, kwani mwalimu mmojaanafundisha takribani masomo 10 kwa siku moja,” alisema.

Hata hivyo, ofisa tawala wa wilaya ya Same, Sospeter Magonera alisema uchache wa madarasa ni changamoto ya shule hiyo na kupitia bajeti ya halmashauri wanatarajia kutenga fedha ili yajengwe.

Magonera anasema serikali inatoa kipaumbele kwenye shule za pembezoni ila watawashirikisha jamii ya eneo hilo ambayo ina utajiri wa mifugo ichangie ujenzi ili serikali iiunge mkono kuliko kuiachia serikali
pekee.

“Suala la walimu nalo litapatiwa ufumbuzi kwani hivi karibuni kuna
ajira mpya za walimu 52,000 zilizotengwa na tunatarajia wale wa Same baadhi yao watapangiwa shule hii,” alisema Magonera.

WALIA NA MPAKA WA EPZ

Baadhi ya watu wanaopakana na eneo huru la biashara la uwekezaji la (EPZ) Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wameiomba Serikali kubainisha mpaka kwani uliopo umeingilia sehemu yao.
 
 Wakazi hao wanadai kuwa mpaka halali wa eneo la EPZ ni hekta 510.64 na siyo hekta 530.87 kama zinavyobainishwa kwani mpaka uliokuwepo awali unaonyesha hivyo na vibao vipo hadi hivi sasa.
 
Wakizungumza jana, wananchi hao walidia kuwa walifikisha kilio chao kwa Waziri mkuu Kasimu Majaliwa alipofanya ziara yake mkoani Manyara,  mwezi Februari mwaka huu na kufika Mirerani.
 
Mchungaji Michael Mtero alisema Waziri mkuu Majaliwa alimuagaiza mkuu wa mkoa huo Dk Joel Bendera afuatilie mgogoro huo na kuupatia ufumbuzi hivyo wanahitaji kujua hatima ya suala hilo.
 
“Mimi nilipatiwa eneo hili ili nijenge kanisa na muumini mmoja ambaye alijitolea sadaka kiwanja chake ila naambiwa kuwa sehemu ya uwanja ipo katika mpango wa EPZ,”  alisema mchungaji Mtero.
 
Blasto Mosses alisema alijenga nyumba baada ya kuuziwa eneo hilo na kupata nyaraka halali kutoka serikalini lakini anashangazwa kuambiwa kuwa nyumba na kiwanja kipo ndani ya sehemu ya EPZ.
 
Israel Loserian alisema hivi sasa wameshikwa na sintofahamu ya tatizo hilo kwani ni muda mferu walikuwa wanamiliki maeneo yao na hivi karibuni kuambiwa kuwa wapo ndani ya uwekezaji wa EPZ.
 
Michael Lekopito (95) alisema alizaliwa kwenye eneo hilo lakini anashangazwa kuambiwa kuwa wamevamia sehemu hiyo ambayo hawakulipwa fidia yao kama baadhi ya watu walivyolipwa.
 
Hata hivyo, mkuu wa wilaya hiyo mhandisi Zephania Chaula alisema waliopo kwenye eneo hilo wapo kimakosa kwani mpaka unaonyesha kuwa wameingia ndani ya na walishawaambia waondoke wenyewe.
 
Mhandisi Chaula alisema walishawaeleza waliouziwa sehemu hiyo wabomoe, kwani awali serikali ilileta mpimaji wakagoma, wakamleta mpima wao akasema wapo ndani ya eneo, hata fedha hawakumlipa.
 
“Hivi sasa wizara ya Nishati na Madini inatarajia kujenga jengo lao kubwa la madini house kwenye eneo hilo na pia tunatarajia kuweka mtaro ili kubainisha vizuri mpaka wa EPZ,” alisema mhandisi Chaula.

Saturday, 20 May 2017

HAKI MADINI KUANDAA MDAHALO



Wachimbaji wadogo wa madini, wachuuzi na madalali wa madini nchini wanatarajia kufanya mdahalo wa kitaifa juu ya umuhimu wa sekta ya madini na namna ya kuwanufaisha zaidi.

Mkurugenzi wa shirika la Haki Madini Amani Mhinda, akizungumza mji mdogo wa Mirerani na viongozi wa chama cha wachimbaji madini mkoani Manyara (Marema) alisema mdahalo huo utafanyika mkoani Geita.

Mhinda alisema lengo la mdahalo huo ni kuwaleta wadau mbalimbali kwa pamoja ili kuzungumzia changamoto zinazoikabili sekta hiyo kwa wachimbaji wadogo na kutafakari kitaifa maono ya wachimbaji.  

Alisema wanatarajia kufanya mdahalo huo mwishoni mwa mwezi Juni kwa kushirikiana na shirika kiongozi duniani la maendeleo la International Institute for Environment and Development (IIED).



“Haki madini tunarajia mpango huu utatoa jukwa hitajika kwa wadau kushirikiana na kubadilishana ujuzi na kukuza utawala bora kuwa sauti kubwa, usalama na utengenezaji,” alisema Mhinda.

Alisema uchimbaji mdogo wa madini unaweza kutoa mchango chanya wenye umoja na usawa wa maendeleo endelevu na ukuaji wa uchumi, kwani husaidia mamilioni ya watu hasa wanawake na watoto.

Katibu wa Marema Tawi la Mirerani, Abubakari Madiwa alisema kupitia mdahalo huo wanatarajia wachimbaji mdogo kunufaika kwa kujengewa uwezo hivyo wamejiandaa kushiriki mara utakapofanyika.

“Haki madini imekuwa msaada mkubwa kwa wachimbaji madini wadogo kwani tumekuwa pamoja bega kwa bega kwa kuhakikisha wachimbaji wadogo wanapata haki zao,” alisema Madiwa.

MBUNGE MARTHA UMBULLA



Mbunge wa Viti maalum Mkoani Manyara, Martha Umbulla akizungumza na wanachi wa Mji mdogo wa Haydom juu ya kuwezesha vikundi vya maendeleo.