Saturday, 20 May 2017

DED MBULU HUDSON KAMOGA



Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Hudson Starnley Kamoga akizungumza na wananchi wa mji mdogo wa Haydom juuu ya kuchangia maendeleo yao.

DC MBULU AWAASA WANANCHI



Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Chelestino Mofuga amewataka wakazi wa Kijiji cha Guye kuacha malumbano na kujenga madarasa ya shule ya msingi kwa muda wa mwezi mmoja.

Mofuga akizungumza na wananchi wa kijiji hicho, alisema anahitaji apatiwe mpango wa maendeleo wa kijiji, apatiwe taarifa hiyo ofisini kwake ikiwemo kujenga madarasa kwa mwezi mmoja.

Alisema pamoja na serikali kuwa na sera ya elimu bure na elimu bila malipo lakini wananchi wanapaswa kujenga madarasa ya shule ili wanafunzi wao waweze kupata elimu kwenye mazingira mazuri.

“Ni kijiji cha ajabu kweli kweli, yaani ninyi mnakaa mwaka mzima lakini hakuna shughuli za maendeleo, kule watoto wanasoma wenu wanasoma kwa mazingira magumu ya madarasa,” alisema Mofuga.

Alisema endapo kuna mapungufu mengine kwenye shule hiyo ikiwemo nyumba za walimu, wananchi hao wanapaswa kuhakikisha yanajengwa kwani hiyo ni kwa jaili ya faida ya watoto wao.

Mkazi wa kijiji hicho cha Guye, John Akonaay alisema anasikitishwa na kitendo cha baadhi ya wananchi wa kijiji hicho kuwa na mwamko mdogo wa kuchangia kutokana na ufujaji wa fedha uliofanyika.

“Tunashukuru mkuu wa wilaya leo (juzi) umeagiza yule mtendaji wa kijiji aliyefuja fedha zetu amekuja na kujibu tuhuma kuwa atazilipa ila tukichanga tena huyu mtendaji mpya asizifuje,” alisema Akonaay.

Mkazi mwingine wa kijiji hicho Adam Sule alisema anasikitishwa na kitendo cha kuambiwa kuwa wakili aliyekuwa anafuatilia kesi ya ufujaji wa fedha za kijiji anawadai sh1.5 milioni hivyo walipe.

“Tulishamlipa huyo mwanasheria lakini hivi sasa bado tunaambiwa tunadaiwa ili hali kwenye taarifa ya awali inaonyesha alishalipwa sh150,000 ya usafiri wa kutoka Babati hadi hapa,”  alisema Sule.

MWISHO.

Friday, 7 April 2017

WATAKIWA KUWAUNGA MKONO WAWEKEZAJI



Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, Jackson Sipitieck amewataka wakazi wa Mji mdogo wa Mirerani kuwapa ushirikiano wawekezaji wa TanzaniteOne na siyo kuwabeza.

Sipitieck amesema wananchi wa mji mdogo wa Mirerani wanapaswa kuwa wazalendo kwa kuwaunga mkono na kushirikiana na wawekezaji wa kampuni ya TanzaniteOne kuliko kuwavunja moyo.


Aliyasema hayo juzi wakati akiushukuru uongozi wa kampuni ya TanzaniteOne waliotoa ahadi ya msaada wa kujenga madarasa saba ya shule ya msingi Songambele ambayo madarasa yake yaliharibika.

Alisema baadhi ya wananchi wa eneo hilo wamekuwa na kigeugeu kwani wakati mwingine kuwabeza wawekezaji hao na siku inayofuata huisifu TanzaniteOne, hivyo wawe na msimamo mmoja unaoeleweka.

“Nadhani ifike mwisho kwa wananchi kuwabeza wawekezaji ambao hutumia nafasi yao kwa kusaidia jamii katika baadhi ya miradi, kupitia kile wanachokipata kwenye uwekezaji huo,” alisema Sipitieck.

Alisema awali halmashauri hiyo ilitaka kuhamisha shule hiyo ambayo tangu mwaka 2013 iliharibika baada ya kupitiwa na mafuriko makubwa ila kampuni hiyo imeahidi kuijenga upya kwa ubora zaidi.




Mkurugenzi wa kampuni ya TanzaniteOne Faisal Shabhai alisema ana imani kubwa kuwa wataendelea kushirikiana jamii ya eneo hilo na kampuni hiyo katika kuhakikisha wanawezesha miradi ya jamii.

“Hivi sasa tunafungua ukurasa mpya kwa kushirikiana nanyi kama kawaida kwa kuhakikisha kile kidogo tunachokipata tunakigawa kwa jamii inayozunguka sehemu ya uwekezaji wetu,” alisema Shabhai.

Mwenyekiti wa mamlaka ya mji mdogo wa Mirerani Adamu Kobelo alisema wananchi wa eneo hilo wanapaswa kuweka kipaumbele kwenye miradi ya jamii na siyo mtu mmoja mmoja kupewa fedha.

Mmoja kati ya wakazi wa eneo hilo, Japhary Matimbwa alisema anaishukuru kampuni ya TanzaniteOne kwa kusaidia baadhi ya miradi ikiwemo kuichimbia kisima shule ya awali na msingi Kazamoyo.


“Wapo watu ambao kipindi cha uwekezaji wa mzungu walikuwa wanapiga bomu na kujinufaisha wenyewe ila sasa hivi wamekuja wawekezaji wazuri ila wachache wanapinga,” alisema Matimbwa.

Wednesday, 5 April 2017

MJASIRIAMALI EMBOREET



Mjasiriamali wa Kijiji cha Emboreet Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, Estar Lemwanda akizungumza juu ya changamoto ya ujasiriamali kwenye eneo hilo ili kujiinua kiuchumi.